WALIMU 1,952 WALIFUNGULIWA MASHAURI YA KINIDHAMU


 NA ASHA MWAKYONDE, DODOOMA

JUMLA ya walimu  1,952 walifunguliwa mashauri ya kinidhamu katika mashauri yaliyofunguliwa 1,362 sawa na asilimia 69.8 ya mashauri yote yalihusu utoro katika kipindi cha mwezi Machi, 2021 hadi Septemba, 2022.

Hayo yasemwa Oktoba 27, 2022  jijini Dodoma na Katibu wa Tume ya Utumishi  wa Walimu (TSC), Mwalimu Paulina Nkwama wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu utekelezaji wa taasisi na vipaumbele vyake kwa  mwaka  2022/2023 amesema mashauri 260 sawa na asilimia 13.3 ya mashauri yote yalihusu kughushi vyeti na mashauri 119 sawa na asilimia 6.1 yalihusu mahusiano ya kimapenzi na wanafunzi.

Ameeleza kuwa mashauri 98 sawa na asilimia 5 yalihusu ukaidi, mashauri 66 sawa na asilimia 3.4 yalihusu ulevi, Mashauri 16 sawa na asilimia 0.8 yalihusu ubadhirifu na mashauri 31 sawa na asilimia 1.6 yalihusu makosa mengineyo. 

Katibu huyo ameongeza kuwa katika mashauri  1,642 yaliyoamuliwa; Walimu 919 sawa na asilimia 56 ya adhabu zilizotelewa walifukuzwa kazi, Walimu 234 sawa na asilimia 14.3 hawakupatikana na hatia, Walimu 115 sawa na asilimia 7 ya adhabu zilizotolewa walishushwa cheo, Walimu 89 sawa na asilimia 5.4 walikatwa mshahara asilimia 15 kwa muda wa miaka mitatu na Walimu 143 sawa na asilimia 8.7 walipewa adhabu ya Karipio.

"Walimu 59 sawa na asilimia 3.6 walipewa adhabu ya Onyo na Walimu 77 sawa na asilimia 4.7 walipewa adhabu ya kufidia hasara.  Mashauri 310 yapo katika hatua mbalimbali za kuyahitimisha (92 uchunguzi na vikao 218),"amesema Mwalimu Paulina.

Mwalimu Paulina amefafanua kuwa Sheria ya TSC itoa haki kwa mwalimu kukata rufaa pale ambapo hakubaliani na uamuzi uliotolewa na Mamlaka yake ya nidhamu au Mamlaka yake ya rufaa. 

Ameeleza kuwa mwalimu asiporidhika na uamuzi wa Mkuu wake wa Shule ambaye ni Mamlaka yake ya kwanza ya nidhamu kwa makosa mepesi ana haki ya kukata rufaa TSC ngazi ya wilaya na kuendelea na ngazi zingine.

Katibu huyo amebainisha kwamba kipindi cha mwezi Machi, 2021 hadi Septemba, 2022; Tume hiyo  ilitoa uamuzi wa jumla ya rufaa 253 zilizopinga uamuzi uliotolewa na mamlaka ya nidhamu.

Aidha amesema kipindi hicho, TSC Makao Makuu ilipokea nakala ya rufaa 64 zilizokatwa kwa Rais kupinga uamuzi wa Tume. Tume iliandaa mwenendo na vielelezo vya rufaa 56 na kuwasilisha kwa Rais, Aidha, Tume inaendelea kuandaa mwenendo na uchambuzi wa rufaa 8 zilizobaki kwa hatua ya kuwasilishwa.

Katika hatua nyingine amesema kuwa kipindi cha miaka mitatu (2020/2021; 2021/2023; 2022/2023) mfululizo bajeti ya Tume hiyo  imeendelea kuongezeka kutoka shilingi Bilioni 14.773 , 14.980 na 15.454 sawia. 

"Hii ni kazi kubwa inayofanywa na Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania," ameongeza.

Ujenzi wa Mfumo wa Tume wa Kielektroniki ujulikanao kwa jina la Teachers Service Commission Information Management System (TSC-MIS), ambapo jumla ya Moduli sita zimekamilika, wataalamu wamezifanyia majaribio na mafunzo yamefanyika kwa watumiaji wa majaribio (pilot) ambako Mfumo utaanza kutumika kwa majaribio katika Wilaya 24 nchini ambapo Shilingi  609,840,000.00 zimetumika katika ujenzi wa mfumo huo," amesema. 

MAFANIKIO 

Amewakaribisha kuwa Tume imefanikiwa kutekeleza majukumu mbalimbali ambayo yameendelea kuboresha mazingira ya Walimu na Sekta ya Elimu kwa ujumla ktika kipindi cha kuanzia Machi, 2021 hadi Septemba, 2022. 

"Jumla ya Walimu 16,749 waliajiriwa, wakiwemo 8,949 wa Shule za Msingi na 7,800 wa Shule za Sekondari na jumla ya Walimu 15,802 walisajiliwa, Walimu wa Shule za Msingi walikuwa 8,512na Sekondari walikuwa 7,290," amesema.

Ameongeza jumla ya Walimu 16,749 waliajiriwa, wakiwemo 8,949 wa Shule za Msingi na 7,800 wa Shule za Sekondari na jumla ya Walimu 15,802 walisajiliwa, Walimu wa Shule za Msingi walikuwa 8,512na Sekondari walikuwa 7,290.

Katibu huyo ameeleza kuwa Rais Samia Suluhu Hassan amefanya kazi kubwa kuhakikisha kila Mwalimu aliyestahili amepanda cheo huku akisema zoezi hilo ni endelevu.

Tume imekuwa ikishughulikia changamoto ya mwalimu mmoja mmoja kwa wale ambao wamekuwa wakilalamika kucheleweshwa kupandishwa madaraja miaka iliyopita ili kuhakikisha kwamba kila mwalimu anapata anachostahili. 

VIPAUMBELE VYA TSC

Mwalimu Paulina amesema Tume hiyo ina vipaumbele vitatu ikiwam kusimamia Utumishi na Maendeleo ya Walimu kwa kudumisha Maadili na Nidhamu kwa Walimu wa Shule za Msingi na Sekondari katika Utumishi wa Umma na itahakikisha Walimu wenye sifa ya kupandishwa vyeo na kubadilishiwa kazi wanapata huduma hiyo kwa wakati baada ya kibali kutolewa na Mamlaka husika.

Amesema Kipaumbele kingine ni juendelea na ujenzi wa jengo la Ofisi za Tume Makao Makuu na kufuatilia ukamilishaji wa Muundo wa Maendeleo ya Utumishi na Mishahara wa Tume pamoja na kuanza kutumia Mfumo wa Kielektroniki wa Usimamizi wa Masuala ya Utumishi wa Walimu kwa majaribio na kuendelea kutoa elimu kwa watumiaji wa Mfumo huo kuanzia ngazi ya Shule.

"Tume itaendelea kuboresha mazingira ya kazi kwa Watumishi  kwa kuwaongezea ujuzi, kuwapatia ofisi na vitendea kazi na kuongeza uelewa kwa Wadau kuhusu Tume ya Utumishi wa Walimu na majukumu yake," ameeleza.

Post a Comment

0 Comments

CHATANDA:RAIS DK. SAMIA AMEIMARISHA SEKTA YA MADINI