BIMA YA AFYA ITALETA USAWA KWA WANANCHI:DKT. SHEKALAGHE

Na Catherine Sungura,WAF-DSM

IMEELEZWA kuwa Bima ya Afya kwa Wote itasaidia kuondoa umaskini na kuinua uchumi wa nchi miongoni mwa wananchi wa Tanzania.

Akiongea kwa njia ya mtandao(Zoom) kutoka  Dodoma Naibu Katibu Mkuu,Wizara ya Afya Dkt. Seif Shekalaghe wakati wa kikao cha kuwajengea uelewa kuhusu Bima ya Afya kwa Wote (UHI) viongozi wa mashirika binafsi na ya umma kikao kilichofanyika leo jijini Dar es Salaam.

Dkt. Shekalaghe amesema kuwa Bima ya Afya kwa Wote itawasaidia wananchi    kwasababu kila mtu atakua na uhakika wa matibabu na hivyo kutokupoteza muda wa kutafuta fedha za kuchangia   matibabu wakati anapokuwa mgonjwa.

"Kila mmoja akielewa umuhimu wa Bima ya Afya kwa Wote,atafanya kazi na kupata  fedha ya kuchangia kabla ya kuugua hivyo pindi anapopata matatizo hatopoteza muda wake na hivyo uchumi wake hautoteteleka".

Hata hivyo amesema Tanzania  sio nchi ya kwanza Afrika  ya  kuwa na mfumo huo na kuongeza kuwa nchi zinazotekeleza mfumo huo zimefanikiwa.

Aidha, Dkt. Shekalaghe aliongeza kuwa Bima ya Afya kwa Wote italeta usawa   kwani kila mmoja atakua na uhakika wa matibabu yeye na familia yake.

"Wananchi wanahitaji elimu ili waelewe umuhimu wa kuwa na  Bima ya Afya ninyi kama wadau wakubwa wa Serikali mtatusaidia hili kupitia wadau wenu hadi ngazi zote hadi  vijijini".

Vilevile Dkt.Shekalaghe amesema Serikali inathamini mchango wa sekta binafsi hivyo kwa kushirikiana wataweza kuwasaidia wananchi wote kwani sote ni mashahidi na wanaona ndugu zao wakipoteza maisha kwa kutokuwa na fedha hivyo Bima ya Afya kwa Wote ni muhimu na uhakika wa kupata matibabu .

Wakichangia Mada zilizowasilishwa na Sekretatieti ya maandalizi ya Muswada wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote wadau hao wameipongeza Serikali kwa hatua hiyo ambayo inaenda kuwasaidia wananchi kutokupata kikwazo cha matibabu pindi wanapougua  kwakuwa watakuwa na Bima ya Afya.

Post a Comment

0 Comments

 MAGARI 25 YA TUME YA MADINI YAMEZINDULIWA,YATASAMBAZWA KWENYE OFISI ZA MAAFISA MADINI