WAATHIRIKA 1,338 WALIOKUWA WAKITUMIKISHWA NDANI NA NJE YA NCHI WAOKOLEWA

Na Asha Mwakyonde,Dodoma 

WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhandisi Hamad Masauni amesema Sekretarieti ya Kuzuia na Kupambana na Usafirishaji Haramu wa Binadamu  imefanikiwa kuokoa na kusaidia waathirika 1,338  waliokuwa wakitumikishwa ndani na nje ya nchi ambapo kati ya hao 1,211  waliokolewa hapa nchini na waathirika  127 walitoka nje ya nchi za Thailand,India,Oman, Yemeni, Kenya, Botswana, Malaysia na Iraq.

Akizungumza jijini hapa leo  Aprili 15,2024 wakati akitoa taarifa ya mafanikio ya Wizara hiyo katika kipindi cha miaka 60 ya Muungano wa Jamhuri wa Tanzania Waziri Mhandisi Masauni  amesema  kati ya waathirika 1,338 waliookolewa  1,290 ni wanawake na 48 ni wanaume.

" Waathirika wote walipewa huduma muhimu zikiwamo malazi, matibabu, chakula, msaada wa kisheria ,urekebishaji  na kuunganishwa na familia zao.

Pia Waziri Mhandisi Masauni ameeleza kuwa Sekretarieti hiyo imefanikiwa kufanya oparesheni za kusambaratisha mitandao inayojihusisha na usafirishaji haramu wa binadamu ambapo kupitia oparesheni hizo wahalifu 218 walikamatwa na kesi 131 zilifunguliwa katika mahakama mbalimbali nchini.

Amefafanua kuwa kati ya kesi hizo 107 zimeshatolewa uamuzi  na wahalifu 81 walipatikana na hatia  ambapo walipewa adhabu ikiwamo kifungo gerezani.

"Wizara kupitia Sekretarieti imefanikiwa kuanzisha Ofisi ya Kuzuia na Kupambana na Usafirishaji Haramu wa Binadamu -Zanzibar ili kuimarisha mapambano dhidi ya biashara haramu ya usafirishaji haramu wa binadamu," amesema  Waziri, Mhandisi Masauni.

Ameongeza kuwa Wizara hiyo kupitia Sekretarieti imefanikiwa kuanzisha Mfuko wa Kupambana na Usafirishaji Haramu wa Binadamu ( The Ant- Trafficking Fund), ili kuimarisha huduma zitolewazo kwa waathirika hao.

Waziri, Mhandisi Masauni ameeleza mfuko huo ni mahsusi kwa ajili ya kusaidia waathirika tu na  unapata fedha kutoka serikalini  na kwa wadau mbalimbali wakiwamo watu binafisi ambapo umeenzishwa kwa mujibu wa kifungu cha 25 cha Sheria  ya Kuzuia na Usafirishaji Haramu wa Binadamu Namba 6/2008.

Post a Comment

0 Comments

CHATANDA:RAIS DK. SAMIA AMEIMARISHA SEKTA YA MADINI