UDOM KUANZISHA KAMPASI MPYA NJOMBE

Na Asha Mwakyonde,Dar es Salaam 

CHUO Kikuu cha Dodoma (UDOM) kinatarajia kufungua kampasi mpya katika Mkoa wa Njombe itakayoanza kutoa mafunzo mwaka wa masomo 2026/2027 ambapo ujenzi wake utatekelezwa kupitia fedha za mradi wa Hits.

Pia kupitia mradi huo chuo kilipokea Dola za Marekani milioni 23 ambapo zinatumika kujenga miundombinu ya madarasa, maabara na kufungua kampasi hiyo mpya katika Mkoa wa Njombe.

Akizungumza Julai 3,2024 jijini Dar es Salaam kwenye Maonesho ya 48 ya Biashara ya Kimataifa maarufu Sabasaba Naibu Makamu Mkuu wa chuo hicho (Mipango, Fedha na Utawala), Profesa Wineaster Anderson, alieleza kuwa Kampasi hiyo itajikita kutoa mafunzo katika eneo la misitu, madini, uvuvi na kuziboresha zaidi sekta zilizoko katika mkoa huo na itatoa ajira kwa Watanzania.

Aidha amesema katika maonesho yam waka huu wameleta bidhaa mpya ambazo zimetengenezwa na wanafunzi pamoja na wanataaluma kupitia tafiti mbalimbali walizofanya.

“Tafiti zetu zimejikita katika jamii ya Watanzania na kutatua matatizo yaliyoko katika jamii yetu Tanzania, kuna mashine ambazo zinasaidia katika sekta ya samaki na  wanafunzi wetu wameingia katika uwanja wa kutengeneza ‘rockets’ na kwenye maeneo ya vyakula ili kutibu maradhi mbalimbali kwa kutumia lishe asili,” ameeleza.

Ameongeza kuwa mafanikio yaliyopo katika chuo hicho yamechangiwa na kuwepo kwa miundombinu mizuri ya kujifunzia na kufundishia hatua inayowawezesha wanafunzi wanaofika chuoni hapo kufanya vema katika masomo yao. 

Post a Comment

0 Comments

CHATANDA:RAIS DK. SAMIA AMEIMARISHA SEKTA YA MADINI