TATIZO LA FIGO HUCHANGIA ASILIMIA 70 WATOTO KUPATA SHINIKIZO LA DAMU


 Kifaa cha kupimia ugonjwa wa shinikizo la damu

Na Asha Mwakyonde

DAKTARI Bingwa wa Magonjwa ya Moyo kwa Watoto kutoka Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI),Dk.Sulende Kubhoja amesema kuwa kati ya watoto 100 wenye ugonjwa wa shinikizo la damu la juu (Hypertension), asilimia 70 wanatokana na tatizo la Figo.

Akizungumza jijini Dar es Salaam hivi karibuni daktari huyo amesema kuwa watoto wachanga wanaozaliwa ambao hawajamaliza siku 40 nao wanapata ugonjwa huo wa shinikizo la damu la juu.

Daktari huyo ameeleza kuwa watoto wanatofautiana umri katika kupata tatizo la shinikizo la damu la juu na kwamba ugonjwa huo kwa mtoto hawezi kugungulika hadi kufanyiwa vipimo.

" Hakuna namba maalumu kama ilivyo kwa watu wazima mfano  120 chini ya 80, kwa watoto inategemea na uzito wengine wanazaliwa na kilo gramu  mbili na nusu, 3,4, hadi 5, kuna vitu vingi vinaangaliwa," ameeleza Dk. Kubhoja.

MFUMO WA MAISHA

Daktari huyo amefafanua kuwa kwa sasa katika taasisi hiyo wanaona kundi jingine la watoto kutokana na mfumo wa maisha kubadilika.

" Mtoto akiamka asubuhi anakaa kuangalia runinga (TV), anachezea simu ya kiganjani kazi za kujishughulisha hamna hachezi kwa sababu hakuna viwanja vikubwa vya kuchezea, shule anayoenda anapelekwa kwa gari anaongezeka uzito," amesema daktari huyo.

Ameongeza kuwa hilo nalo ni kundi jingine la watoto wanaopata ugonjwa wa shinikizo la damu la juu ndio mambo yanayotokea kwa watu wazima yanatokea kwa watoto hivyo anaweza hata kupata ugonjwa wa kisukari.

Dk. Kubhoja ameeleza  kuna familia ambazo zinajulikana kuwa baba au mama ana shinikizo la damu la juu  wanawaona watoto ambao hawajafikisha umri wa miaka 18 wanapata tatizo la ugonjwa huo. 

Amefafanua kuwa shinikizo la damu la juu haliji ghafla mara moja bali linakuja taratibu  kama vile mwanadamu anavyokua hivyo basi kadri mtoto  anavyokua anaongezeka uzito ndivyo ugonjwa huo unavyokua.

"Tunaweza sema ni mfumo wa maisha umesaidia kuchangia. Ukigundua mapema na maisha yakabadilika," amesema.

Ameongeza kuwa watoto ni Taifa la kesho hivyo wapimwe  mara kwa mara ili kuepuka tatizo hilo kwani wanavyoenda hospitali kwa tatizo jingine ndio anagundulika na ugonjwa wa shinikizo la damu la juu.

Post a Comment

0 Comments

CHATANDA:RAIS DK. SAMIA AMEIMARISHA SEKTA YA MADINI