DK.FATMA:VIONGOZI WA DINI TOENI ELIMU KUPINGA UKATILI



Kamishna wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB),Dk. Fatma  Khalfan.

Na Asha Mwakyonde, Dodoma

KAMISHNA wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB),Dk. Fatma  Khalfan amewataka  viongozi wa dini  kuendelea kutoa elimu ya kiroho kwa wananchi ili kujiepusha na vitendo vya ukatili dhidi ya watoto wanapokuwa katika nyumba za ibada huku 
akiwataka pia wazazi kuwajibika  katika kuwapa watoto malezi bora yenye kuzingatia maadili na desturi za kitanzania na kumlinda mtoto dhidi ya vitendo vya ukatili na udhalilishaji; 

Hayo ameyasema jijini Dodoma Juni 16 , 2022 wakati akitoa tamko katika kilele cha Maadhimisho ya siku ya Mtoto wa Afrika Duniani yalifanyika katika viwanja vya Nyerere Skwea yenye kauli mbinu  isemayo “Tuimarishe ulinzi wa Mtoto; Tokomeza Ukatili Dhidi Yake: Jiandae kuhesabiwa" kwa niaba ya Makamu Mwenyekiti wa (THBUB) Mohamed Khamis Hamad  amesema kuwa 
vyombo vya kusimamia sheria  navyo vichukue hatua madhubuti dhidi ya watuhumiwa wanaojihusisha na vitendo hivyo  vya ukatili.
Amesema kuwa THBUB inatambua na kupongeza jitihada mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali ya Jamhuri wa Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kulinda na kukuza haki za mtoto ikiwemo kuanzisha madawati ya Jinsia na Watoto katika Vituo vya Polisi, upatikanaji wa huduma ya afya kwa mama na mtoto.

Kamishna huyo ameeleza kuwa jitihada hizo ni pamoja  na kuanzisha mahakama maalum ya kushughulikia mashauri ya udhalilishaji kwa wanawake na watoto Zanzibar, kuwarejesha watoto wa kike waliopata ujauzito katika mifumo ya elimu, kuanzisha kamati za ulinzi wa mtoto nchini na kukemea ukatili wa kijinsia kwa watoto.

Ameongeza kuwa  kwa upande wake tume hiyo imeendelea kutoa elimu kuhusu haki za watoto kupitia matamasha ya watoto na vilabu vya haki za binadamu na utawala bora ilivyoanzisha kuanzia ngazi ya shule za msingi hadi vyuo vikuu. 

Kamishna huyo amesema tume imeendelea kuhamasisha jamii kujiepusha na vitendo vya ukatili dhidi ya watoto kupitia vipindi vya radio,  runinga (TV),semina, na maadhimisho.

" Pamoja na jitihada hizi bado kumekuwepo na changamoto kadhaa, ikiwemo watoto kuendelea kufanyiwa ukatili wa kingono, kupigwa, kutelekezwa na kuuawa, uelewa mdogo kwa wananchi kuhusu haki za mtoto, wananchi kumaliza mashauri ya jinai yanayowahusu watoto kifamilia, wananchi kutotoa taarifa juu ya matukio ya ukatili dhidi ya watoto, na uwepo wa mila zenye madhara kwa watoto katika maeneo mbalimbali nchini," amesema Dk.Fatma.

MAPENDEKEZO YA THBUB

Amesema kutokana na changamoto zinazoathiri haki za watoto, THBUB inapendekeza serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali iendelee kutoa elimu kuhusu haki za watoto na athari za ukatili dhidi yao;

Dk. Fatma amefafanua kuwa wadau wa haki za binadamu waendelee kutoa elimu ya haki za binadamu kwa jamii ili kubadili mila na tamaduni potofu 

Aidha amesema kuwa vyombo vya kusimamia sheria vichukue hatua madhubuti dhidi ya watuhumiwa wanaojihusisha na vitendo vya ukatili na 
wananchi kutoa taarifa juu ya matukio yote ya ukatili na udhalilishaji dhidi ya watoto.

"Wadau wote wa haki za watoto waendelee kushirikiana katika kulinda, kuhifadhi na kukuza haki za watoto
THBUB inaahidi kuendelea kutoa ushirikiano kwa Serikali, wananchi na wadau mbalimbali katika kulinda, kuhifadhi na kukuza haki za binadamu na misingi ya utawala bora. 

Ameongeza kuwa tume ume ya inaungana na wadau wote wa haki za watoto katika kuadhimisha Siku ya Mtoto wa Afrika.” Siku hii inaikumbusha dunia juu ya mauaji ya watoto wapatao 2,000 wa kitongoji cha Soweto nchini Afrika Kusini, waliouawa kikatili na iliyokuwa Serikali ya Makaburu.



Post a Comment

0 Comments

CHATANDA:RAIS DK. SAMIA AMEIMARISHA SEKTA YA MADINI