NAIBU WAZIRI MWANAIDI: KUNA UPUNGUFU WA MAOFISA USTAWI JAMII 21,204


 Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake  na Makundi Maalum, Mhe. Mwanaidi Ali Khamis, akifungua Kikao kazi cha kuwajengea uwezo wabunge vinara wa Ustawi wa Jamii kuhusu utekelezaji afua mbalimbali za usimamizi, uendeshaji na utoajj huduma za  ustawi wa Jamii katika Halmashauri kilichofanyika jijini Dodoma, Juni 21, 2022.

Kamishna wa Ustawi wa Jamii Msaidizi Baraka Makona akizungumza kwenye kikao Kazi  cha kuwajengea uwezo wabunge vinara wa Ustawi wa Jamii kuhusu utekelezaji afua mbalimbali za usimamizi, uendeshaji na utoaji huduma za  ustawi wa Jamii katika Halmashauri, kilichofanyika jijini Dodoma Juni 21, 2022.

Kaimu Mwenyekiti wa Chama cha Wataalamu wa Ustawi wa Jamii TASWO,  Joseph Kayinga akitoa maelezo ya awali kuhusu kikao kazi cha kuwajengea uwezo wabunge vinara wa ustawi wa Jamii  kuhusu utekelezaji wa afua mbalimbali za usimamizi, uendeshaji na utoaji huduma za  ustawi wa Jamii katika Halmashauri  kilichofanyika jijini Dodoma Juni 21, 2022.

Mkurugenzi wa Afya, Lishe na Ustawi wa Jamii kutoka Ofisi ya Rais-TAMISEMI Dkt. Ntuli Kapologwe akizungumza wakati wa kikao cha kuwajengea uwezo wabunge vinara wa ustawi wa Jamii kuhusu utekelezaji afua mbalimbali za usimamizi, uendeshaji na utoajj huduma za  ustawi wa Jamii katika Halmashauri kinachofanyika jijini Dodoma Juni 21, 2022.

Baadhi ya wabunge vinara wa Ustawi wa Jamii wakifuatilia hotuba ya ufunguzi wa kikao cha kuwajengea uwezo kuhusu utekelezaji afua mbalimbali za usimamizi, uendeshaji na utoajj huduma za  ustawi wa Jamii katika Halmashauri kutoka kwa Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Mwanaid Ali Khamis kilichofanyika jijini Dodoma Juni 21, 2022

Na Asha Mwakyonde Dodoma 

NAIBU Waziri wa Maendeleo ya Jamii,Jinsia Wanawake na Makundi Malaamu Mwanaidi Ally Khamis amesema kuwa kuna upungufu mkubwa wa Maofisa Ustawi wa Jamii ambapo mahitaji  ni 22,250 lakini waliopo ni 1,046, hivyo upungufu ni 21,204 kuanzia ngazi ya Sekretarieti za Mikoa hadi kijiji na mitaa. 

Hayo ameyasema jijini Dodoma Juni 21,2022 katika Mkutano Kati ya Chama Cha Wataalamu wa Ustawi wa Jamii (TASWO),Wadau na Wabunge Vinara wa Huduma za Ustawi wa Jamii, amesema mahitaji ya Maafisa Ustawi wa Jamii yanalenga kufikisha huduma katika jamii kwa wakati.

Ameeleza kuwa pamoja na kuwepo kwa idadi ndogo ya wataalam hao,waliopo wanakabiliwa na uhaba wa rasilimali fedha na  ukosefu wa vitendea kazi  kuifikia jamii kwa ufanisi.

Naibu Waziri huyo amebainisha kuwa hali hiyo  imesababisha  kuzorota kwa huduma za ustawi wa jamii na Maafisa kushindwa kutekeleza majumuku yao ipasavyo ambapo huenda ikasababisha kuongezeka kwa idadi ya watu au makundi yenye mahitaji maalumu na baadae kupunguza nguvu kazi ya taifa na kuongeza mzigo kwa Serikali.

Amesema huduma za Ustawi wa Jamii zinahitaji kuifikia jamii na makundi yenye mahitaji maalum kwa wakati ili kutatua changamoto zinazowakabili ili washiriki kikamilifu katika ustawi na maendeleo ya taifa.

 "Hata hivyo, kuna idadi ndogo ya Maafisa Ustawi wa Jamii wanaopaswa kusaidiana na watoa huduma wengine kuiwezesha jamii kutatua  changamoto mbalimbali zinazoikabili ikiwemo vitendo vya ukatili wa kijinsia, utelekezwaji na mauaji ya wazee na watu wenye ulemavu, ongezeko la watoto wanaoishi na kufanyakazi mtaani, hali duni ya uchumi wa kaya na familia, tatizo la afya ya akili, migogoro ya ndoa na familia, mmomonyoko wa maadili kutokana na ukosefu wa huduma bora ya malezi, makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto," amesema.

Naibu Waziri huyo amesema kuwa ongezeko la watoto waliokinzana au walio katika hatari ya kukinzana na sheria pamoja na uwepo wa majanga ya dharula yanayotokea katika jamii  kama vile mlipuko wa magonjwa (UVIKO19), ajali, masoko kuungua.

Ameaema maafisa Ustawi wa Jamii wakiajiriwa kwa idadi timilifu katika Mamlaka za Serikali za Mitaa hadi ngazi ya Kijiji na Mtaa, itawezesha jamii kufikiwa kwa wakati ambapo watajengewa ustahimilivu na uwezo wa kukabiliana  na changamoto zinazowakabili ikiwemo kuwa imara katika hali za saikolojia, kuwajibika na kuwa na familia zenye amani na upendo na salama kwa watoto kulelewa.

Sambamba na hayo amesisitiza kuwa pia itasaidia kupunguza ukatili, watoto wanaoishi na kufanya kazi mitaani, watoto wanaokinzana na sheria, mimba za utotoni, migogoro ya kifamilia na ndoa, utelekezwaji wa watoto, watu wenye ulemavu na wazee. 

"Natoa rai kwa kamati kutoa ushauri, hamasa na msukumo zaidi kwa Serikali kuajiri  Maafisa Ustawi wa Jamii  wa kutosha ngazi zote. Nawasihi kuweka msukumo wa ongezeko la bajeti katika Halmashauri zote nchini za rasilimali fedha na vitendea kazi ili maafisa watekeleze  majukumu yao bila vikwazo.

Amesema wataalam hao wakiajiriwa ngazi zote na kuwezeshwa kutekeleza majukumu yao ipasavyo itawezesha kupungua kwa idadi ya watu au makundi  yenye mahitaji maalum au watu wanaoishi katika mazingira hatarishi  kwa vile watawezeshwa kuhitimu  katika hali zao na kujikita katika shughuli za uzalishaji mali na ustawi wa familia zao na hivyo kuchangia katika ukuaji wa uchumi wa nchi.

" Ninawashukuru na kuwapongeza viongozi na watumishi wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maluum, Wizara za Kisekta, watumishi, Mashirika na Asasi za kiraia pamoja na  TASWO, kwa uratibu na utoaji wa huduma za ustawi wa jamii," amesema.

Awali Kaimu Mwenyekiti wa Chama Cha Wataalamu wa Ustawi wa Jamii (TASWO), Joseph Kayinga amesema kuwa mkutano huo  malengo makuu manne na lengo la kwanza ni kuhamasisha Wabunge hao  juu ya umuhimu  wa Ustawi wa Jamii kwa maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa Taifa na kwa mtu mmoja mmoja na makundi maalumu.

Kaimu Mwenyekiti huyo amefafanua kuwa lengo la pili ni kutetea, kusaidia utambuzi  kueleza umuhimu nafasi na majukumu na jitihada zinazochukuliwa na serikali kupitia wizara, Idara na wadau 

Ameongeza kuwa lengo la tatu ni kuwajengea uwezo na uelewa Wabunge hao Vinara wanaunga mtazamo huo wa Ustawi wa Jamii bengeni kuhusu masuala hayo ili inapotokea mchango wa kuchangia waweze kuchangia Kwa upana zaidi.

Kayinga amesema kuwa lengo la nne ni kuhimiza na kusaidia kukuza kuboresha mazingira mazuri ya kazi za Watendaji kuanzia ngazi ya chini hadi juu.

Amesema Chama hicho kinapata huduma  na ushirikiano kutoka serikalini, na kwamba upo uzoefu wa nchi nyinyi za Afrika kati ya serikali zao na Vyama vya kitaaluma  haviendi pamoja lakini kwa Tanzania wanapata ushirikiano.

"Hizi nguzo zote nne zikikamilika na kufanya kazi vizuri sisi kama Wataalamu haki na usawa wa binadamu na maandeleo yote ya jamii yataweza kufikiwa," amesema Kayinga.

Naye Katibu wa Kamati ya Wabunge Vinara wa masuala ya Ustawi wa Jamii ambaye pia ni mbunge Kilolo Iringa Justin Nyamoga  amesema kuwa wao kama Wabunge wamekuwa wakipiga kelele bungeni ili Maofisa Ustawi wa Jamii waongezwe.

"Nawashukuru TASWO kwa kuwajibika ipasavyo katika kutekeleza wajibu wao  wa masuala ya kijamii na kupinga vitendo vya kikatili nasi tutaendelea kuangalia mbali zaidi juu ya Ustawi wa jamii kwa makundi yote," amesema.

" Ninawashukuru na kuwapongeza viongozi na watumishi wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maluum, Wizara za Kisekta, watumishi, Mashirika na Asasi za kiraia pamoja na  TASWO, kwa uratibu na utoaji wa huduma za ustawi wa jamii," amesema.


Post a Comment

0 Comments

CHATANDA:RAIS DK. SAMIA AMEIMARISHA SEKTA YA MADINI