FAHAMU SIRI YA MADALALI KUCHUKUA KODI YA MWEZI MMOJA KWA MPANGAJI


*Wamesema ni mfumo walioukuta ambao si wa kisheria

* Waziri wa Ardhi atoa mkakati wa serikali

Na Asha Mwakyonde

Licha ya serikali kutoa agizo, kupiga marufuku madalali kuchukua kodi ya mwezi mmoja kwa wapangaji lakini bado madalali hao wanaendelea kuchukua kodi hiyo jambo ambalo limekuwa ni changamoto kwa wapangaji hao hali inayosababisha migogoro ya kimya kimya kwa pande hizo mbili.

Agizo hilo lilitolewa na aliyekuwa Waziri wa Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi akiwa Mkoani Iringa Novemba 15 ,2021, alipiga marufuku madalali wanaochukua kodi ya mwezi mmoja kwa wapangaji na badala yake walipwe na wenye nyumba kwa kuwa ndio waliowapa kazi yakuwatafutia wateja.

MPANGAJI

Wakizungumzia changamoto wanazokutana nazo, wapangaji  hao walisema kuwa wamekuwa wakipata adha nyingi hasa pale wanapokutana na madalali kwa lengo la kupatiwa nyumba, vyumba ikiwamo ya kuwalipa kodi ya mwezi mmoja.

Salehe Lujuo ni mpangaji na mkazi wa Chang’ombe jijini Dodoma, ameeleza changamoto, adha wanazokutana nazo kwa madalali hao ya kutaka kodi ya mwezi mmoja jambo ambalo linawaumiza wanapotafuta nyumba,vyumba.

“Angalau madalali wawe wanachukua hata elfu kumi lakini wao wanachukua kodi nzima mfano umepanga nyumba ya laki mbili na nusu kwa mwezi unatakiwa nao uwalipe hiyo, tunaumia sana wapangaji,” amesema Lujuo.

Lujuo amesema kitu kingine kinachowaumiza , madalali sio wa kweli huku akieleza kuwa wanaweza wakasema nyumba nzuri, ina maji, umeme lakini anapofika anakuta ni tofauti na aliyoelezwa.

Akizungumzia agizo la aliyekuwa Waziri wa Ardhi, Lukuvi Lujuo amesema agizo hilo lilikuwa ni siasa ili kiongozi huyo aonekane anafanya kazi na kujiaminisha kwa wananchi wake kuwa anafanyakazi kuwalinda, kuwatetea wanyonge.

“Serikali ingekuwa na msimamo agizo hilI lingefanikiwa kwa kiasi kikubwa lakini  ni siasa na Waziri alitaka kuonekana ni mtatuzi wa kero kwa jamii,”amesema.

Naye Mkazi wa Kikuyu jijini Dodoma, Rehema Ally akizungumzia changamoto za wapangaji kutoka kwa madalali amesema baadhi yao  wanatamaa na fedha wanaweza wakampatia mtu nyumba na kufanya malipo, lakini akitokea mwenye kodi kubwa anarudishiwa kodi yake na kuanza kutafuta tena nyumba nyingine.

“Tunapitia changamoto nyingi kutoka kwa madalali ambao wanaonekana kama wao ndio wamiliki wa nyumba kutokana na makubaliano waliyokubaliana na mmiliki wa nyumba,”ameeleza.

Rehema amefafanua kuwa changamoto nyingine wanayokutana nayo wapangaji ni kuongezewa kodi na madalali huku akieleza kwamba nyumba au chumba kinaweza kuwa kodi yake ni bei ya chini lakini dalali kwa maslahi yake anapandisha kiwango cha kodi hiyo tofauti na kile cha mwenye nyumba.

WITO WAO KWA SERIKALI

Lujuo ameishauri serikali kutengeneza utaraibu mzuri utakaotumiwa na madadali pamoja na wapangaji huku akitolea mfano mpangaji anahitaji chumba kimoja cha shilingi elfu 50 dalali apatiwe elfu 10 au 15,000.

Pia amewataka wenye nyumba kuwalipa madali kwa kuwa ndio waliowapatia kazi ya kuwatafutia wateja na si kumuumiza mpangaji kwa kutoa kodi ya mwezi mmoja.

“Asilimia kubwa ya wenye nyumba wanawaachia madalali kama matajiri wao wafanya maamuzi ya kupanga kodi wao bila kujali maumivu anayoyapata mpangaji, inakuwa ni biashara,” amesema Lujuo.

Pia mpangaji huyo ameishauri serikali kupitia serikali za mitaa kufanya tathmini ya viwango na ubora wa nyumba pamoja na kuweka kodi halisi kutokana na nyumba husika hivyo mpangaji atakapofika katika serikali hiyo atachagua nyumba gani na ya kodi kiasi gani anayotaka kuishi.

WAMILIKI WA NYUMBA

Wakizungumzia makubaliano yao kati ya mwenye nyumba na dalali walisema  kila mtu ana nyumba  yake ndivyo  hivyo sheria zinatofautiana  hata katika makubaliano ndivyo hivyo.

Mkazi wa Ilazo jijini Dodoma Amina Lema akizungumzia makubaliano kati ya dalali na mwenye nyumba anapotaka kutafutiwa mpangaji ameeleza dalili  hupita kuulizia nyumba, chumba ambacho mtu amehama na akifanikiwa kupata ataomba funguo za nyumba, au kufanya makubaliano na kuanza kutafuta mpangaji.

"Hatuna makubaliano yoyote na dalali isipokuwa anakuwa kama mfanyabiashara mchuuzi anayenunua bidhaa kwa bei ya jumla halafu anaenda kuuza bei ya reja reja  hata  akimpata mpangaji wanakubaliana wenyewe mimi sihusiki na sitampa hela yoyote," ameongeza.

Mfano chumba napangisha 60,000 na nataka ilipwe kodi ya miezi sita bado dalali ataongeza kodi ya nwezi mmoja  ambayo atachukua yeye lakini mi sitajua makubaliano yao, " amesema Amina.

Hata hivyo mmiliki huyo  wa nyumba amezungumzia changamoto wanazokutana nazo kutoka kwa madalali amesema dalali anaweza kwenda kumpangisha jambazi, mtu mwenye matatizo, msumbufu na hata kama akikuta masharti , utaratibu wa nyumba huku akitolea mfano namna ya ulipaji bili za maji, takataka na umeme atakataa baada ya kuingia licha ya kusaini mkataba.

Naye Jumanne Hassan ameseleza kuwa kama mmiliki wa nyumba huwa anamwambia dalali akimpata mteja ampeleke suala la kodi ni baina yeke na mteja kutokana na baadhi yao kutokuwa waaminifu.

KUHUSU UMOJA WA WAMILIKI WA NYUMBA

wakizungumzia suala la umoja, Chama cha Wamiliki wa Nyumba wamesema hawana umoja kwa kuwa kila mtu anangalia mali yake ya nyumba na maamuzi  ni yake  kwani suala la upangishaji ni la mwenye nyumba.

"Nyumba ni yangu  naimiliki chini ya himaya yangu uwezo  na masharti ninayo mwenyewe umoja wa nini, umoja haunipi kitu chochote wala msaada wowote, isipokuwa napenda kumtendea mpangaji haki kwani katika maisha kuna leo na kesho, mwanadamu amepewa amana ili imsaidie mwezie siyo uifanye fimbo ya kumuadhibia mtu mwingine," amesema Amina.

KAULI ZA MADALALI

Wamesema kuwa utaratibu, mfumo wa kuchukua kodi ya mwezi mmoja kwa wapangaji pindi wanapowatafutia nyumba wameukuta ingawa haupo kisheria.

Ally Kombo ni dalali  wa Chumba, vyumba mwenye maskani yake katika eneo la Mtendeni jijini Dodoma  akizungumzia makubaliano yake na mwenye nyumba ambayo atamtafutia mpangaji amesema atakwenda katika kijiwe chao au atapiga simu ili kuwajulisha iwapo ana nyumba anayohitaji kupangisha.

"Akija au akipiga simu nitamuuliza ipo sehemu gani, ina ubora gani na anapangisha kwa shilingi ngapi baada ya maswali hayo nachukua kazi nakaa nayo na kuwajulisha wenzangu mteja akipatikana tunampigia mwenye nyumba, mteja ataiona akiipenda watakubaliana na kumlipa kodi yake," amesema Kombo.

Kombo ameongeza kuwa utaratibu waliojiwekea hela ya udalali wanaipata kwa mpangaji kwa kuwa ndiyo mwenye uhitaji na  huo ni mfumo ambao wameukuta hivyo hawawezi kuubadili labda ikiwekewa sheria.

Ameeleza kuwa lazima dalali achukue kodi ya mwezi mmoja ndiyo makubaliano waliyokubaliana ambayo hayapo kisheria  bali ni makubaliano.

Kombo amefafanuua kuwa hakuna mtu yoyote anaeyeenda kununua kitu hajui kama kuna hela ya udalali hata nchi inafanya biashara kwa kupitia madalali.

Naye Mkazi wa Makole jijini hapa Mwasiti Haruna ambaye pia ni dalali  amesema kwa upande wake akimpata mteja wanakubaliana kabisa hela ya udalali ili kuepuka kudhulumiwa na mteja.

AGIZO LA ALIYEKUWA WAZIRI WA ARDHI, LUKUVI

Wakizungunzia agizo, tamko  Lukuvi wamesema kuwa agizo hilo lilikuwa la kisiasa kwani serikali haikuweka miundombinu mizuri ya wao kufanya kazi ya udalali bali viongozi  wanatoa matamko yasiyotekelezeka.

Kwa upande wake Mwasiti amesema alishangazwa na agizo hilo huku akisema viongozi wengi wana nyumba, vyumba mkoani hapa na wao ndio wanaowatafutia wapangaji hawajawahi kutoa hela ya udalili bali wanapewa wapangaji.

KUHUSU CHANGAMOTO

Kombo akizungumzia changamoto amesema kwa kipindi hiki cha sasa kutokana na mfumo wa maisha  ulivyobadilika  madalali wamekuwa wengi kuliko kazi za udalali huku akifafanua kwamba hadi waendesha pikipiki ( Boda boda) na madereva taksi nao wamekuwa madalali.

Amesema kwa mwezi wanaweza wakapata mpangaji, mteja mmoja kwani kutokana na wingi wa madalali wanaopatikana  kila sehemu.

"Lakini changamoto nyingine kubwa ni pale mteja atakapotaka kulipa kwa kutumia 'Invoice' inabidi tuende kwa mtu mwenye kampuni ili fedha zilipwe kupitia akaunti ya kampuni," amesema Kombo.

Dalali Mwasiti ameeleza kuwa kazi ya udalali kwa sasa imekuwa ngumu kwani madalali wamekuwa wengi kuliko wapangaji hata muuza mboga mboga naye  ni dalali hivyo hali hiyo inawasababishia kukosa wateja tofauti na awali.

 UMOJA WA MADALALI

Wakizungumzia kuhusu umoja wa madalali Kombo ameeleza kuwa watanzania ni watu ambao wanashindwa kufanya umoja  na kama utakuwepo utakuwa ni wa familia.

"Kitendo cha kukutana na kukaa kujenga mikakati ya  umoja ukweli ni kwamba Watanzania hatuna umoja kwanza tunakosa uaminifu, ukweli ujanja ujanja  haya yanachangia kutokufanikisha kuwa na umoja ambao utakuwa na nguvu," amesema Kombo.

Mwasiti amesema  hawawezi kuwa na umoja wa madalali kwa kuwa hawaaminiani wenyewe kwa wenyewe hivyo wanaogopa kudhulumiana.

WITO KWA SERIKALI

Kombo ameeleza kuwa kama serikali ina nia thabiti ya kuondoa jambo la wao kuchukua kodi kwa mpangaji iweke mfumo wake vizuri unaoeleweka na kupitishwa kisheria.

"Kwanza serikali  iangalie nyumba zao za serikali zinalipwa kwa tararibu zilizowekwa, wapangaji wanapata kwa taratibu zilizowekwa?….Lakini isitake wananchi kufuata tararibu wakati yenyewe haiwezi," ameeleza Kombo.

Mwasiti amesema wanaipenda kazi hiyo ya udalali iboreshwe ili iheshimike kwa jamii kwa kuwa baadhi yao wanaitegemea kama ilivyo kazi nyingine.

WAZIRI WA ARDHI

Akizungumzia agizo la aliyekuwa Waziri wa Ardhi, Waziri mwenye dhamana Angelina Mabula amesema kuwa kuna sheria inaandaliwa na Wizara ya Fedha na Mipango ambayo itawabana madalali hao hivyo bado wanasimamia tamko la Waziri Lukuvi.

"Kuna sheria inaandaliwa unaweza kutoa katazo kama sheria haipo utekelezaji wake inakuwa ni ngumu kidogo kwa hiyo kuna matamko yanatoka, bado tunasimamia agizo lipo pale pale lakini litasimamiwa zaidi kwa sheria Wizara tusubiri itakapokuwa tayari," ameeleza Waziri huyo.

Aidha Waziri huyo amewataka madalali hao kuacha mara moja kuwadhulumu wananchi wapangaji kwa kuwa kitendo hicho si cha kiungwana.

LHRC

Kwa upande wake, Wakili na Msamizi wa ofisi ya Msaada wa Kisheria  Kinondoni iliyo chini ya Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Rose  Nyatega amesema hakuna sheria inayozungumzia madalali wa nyumba kuchukua kodi kwa mpangaji pindi anapomtafutia nyumba, chumba hivyo hakuna mpangaji anayelazimishwa kutumia dalali wakati anatafuta nyumba.

"Mwenye nyumba halazimishwi kutangaza nyumba yake kupitia dalali ila kiuhalisia dalali yupo kwa makubaliano kama sio ya mwenye nyumba basi mpangaji ukiangalia mtu kutafuta nyumba mwenyewe kutafuta inachukua muda sana kama ambavyo ungetumia dalali ila pia mwny nyumba kutangaza mwenyew inaweza ikachukua muda kupata mteja sio kama ukitangaza kupitia dalali," amesema Rose.

Wakili huyo ameeleza kuwa wao wanapenda kuona haki ikitendeka hivyo serikali ione jinsi ya kuweka sheria ya kuwadhibiti  madalali kwani  wapangaji wengi wanajikuta wanalipa pesa nyingi wanapotaka kupanga na pia utapeli au janja janja unafanyika kwa madalali hao.

Post a Comment

0 Comments

CHATANDA:RAIS DK. SAMIA AMEIMARISHA SEKTA YA MADINI