LISHE DUNI INAVYOCHANGIA UDUMAVU KWA WATOTO


Na Asha Mwakyonde,Dodoma

UDUMAVU kwa watoto walio chini ya umri wa miaka  mitano mara nyingi husababishwa na kutopata lishe bora tangu anapokuwa tumboni mwa mama yake katika siku 1,000 za mwanzo za makuzi ya mtoto huyo.

Kipindi cha  miezi sita ya awali baada ya kuzaliwa mtoto anatakiwa kunyonya maziwa ya  mama pekee bila kuchanganyiwa chakula chochote kwa mujibu wa miongozo ya Wizara ya Afya. 

Baada ya miezi hiyo  mtoto ataanza  kulishwa chakula taratibu kwa kuwa maziwa ya mama pekee hayawezi kumtosheleza mtoto huyo,  hivyo mama ataendelea kumnyonyesha kama kawaida hadi atakapo timiza umri wa miaka miwili na zaidi.

Miongoni mwa sababu kubwa ya vifo  vya watoto walio chini ya miaka mitano,  vinakadiriwa  kugharimu serikali asilimia 2.6 ya pato la taifa, hivyo kutokana na hali hiyo idadi kubwa ya watoto wenye udumavu wa mwili na akili inaelezwa kuwa kubwa kwa taifa.

TAASISI YA  TFNC

Kwa mujibu wa  takwimu zilizotolewa na Taasisi ya Lishe na Chakula Tanzania (TFNC), mwaka 2018 zinaonesha udumavu mkoani Dodoma upo kwa asilimia 37.2, zikiwa  na maana ya kila  watoto 100, watoto 37 wamedumaa.

Pia takwimu hizo hizo, zinaonyesha kwa mwaka 2018, kulikuwa na watoto chini ya miaka mitano 433,576 ambapo 37.2% ya hiyo ni sawa na watoto 161,290.

JITIHADA ZA SERIKALI

Katika kuhakikisha udumavu nchini unapungua Septemba 30, Mwaka huu Rais Samia Suluhu Hassan ameshuhudia utiaji saini wa Mikataba ya usimamizi wa shughuli za lishe kwa Wakuu wa mikoa katika halfa iliyofanyika mkoani Dodoma.

Rais Samia amesema kuna umuhimu wa kuongeza bajeti kwenye lishe ili kuwajengea uelewa zaidi wananchi katika suala la lishe kwa maendeleo ya taifa lengo likiwa ni kupunguza tatizo la vitambi katika  kuendeleza kizazi chenye afya bora.

Pia Rais Samia ameongeza kuwa kuna haja ya  kuipitia upya sera ya lishe ya mwaka 1992 ili iendane na wakati wa sasa na taasisi binafsi za lishe kufuata mpango wa taifa wa lishe .

HALI YA UDUMAVU MKOA WA DODOMA

Rosemary Senyamule, ni Mkuu wa Mkoa wa Dodoma akizungumza  hivi karibuni wakati akisaini  mkataba wa utendaji kazi za lishe baina yake na wakuu wa Wilaya ambao unaratibiwa na kusimamiwa na idara ya afya Mkoa amesema Mkoa huo una tatizo la lishe na kwamba  udumavu upo kwa asilimia 37.

Amesema Lengo kubwa la mkataba huo ni kuhakikisha suala la kuboresha hali ya lishe na kupunguza athari za utapiamlo katika Halmasahauri zote, zinasimamia ipasavyo utekelezaji wa afua za lishe ikiwa ni pamoja na  kuchukua hatua za kupunguza hali duni ya lishe katika halmashauri hizo.

" Tuna kazi kubwa ya kufanya kwa ajili ya kuboresha suala la  lishe katika Mkoa huu tunaambiwa tuna tatizo la lishe kwa  asilimia 37 idadi hii ni kubwa," amesema mkuu huyo wa Mkoa.

Ameongeza kuwa  mkataba huo umepewa uzito na Serikali ndio maana wamesaini huku akiwataka Wakuu hao wa Wilaya kwenda kuutekeleza na kuupa uzito.

UMUHIMU WA LISHE

Akizungumzia umuhimu wa lishe kwa mtoto, Afisa Lishe kutoka Wizara ya Afya Kitengo cha Huduma za Lishe Jenipha Mayenga amesema kuwa katika ukuaji wa mtoto na uwezo, lishe bora huwapa watoto nishati ya kuishi maisha kamili, huwalinda dhidi ya utapiamlo, kudumisha mfumo wa kinga, kuzuia unene na kupunguza hatari ya magonjwa sugu.

Kwa upande mwingine Afisa huyo ameeleza kuwa lishe duni hasa katika siku 1,000 za kwanza za maisha ya mtoto (kuanzia kipindi cha ujauzito hadi mtoto anapofikisha umri wa miaka miwili) inaweza kusababisha matatizo ambayo hayawezi kurekebishika kama kumuweka katika hatari ya udumavu wa mwili na ubongo ambayo huweza kuathiri uwezo wa kufanya vizuri shuleni.

Ameongeza kuwa watoto waliodumaa huwa na uwezo mdogo wa kushiriki, kuhusiana na watoto wengine vizuri katika michezo na maeneo mengine. 

"Lishe duni husababisha kuwa na kinga duni dhidi ya magonjwa hivyo humfanya mtoto augue mara kwa mara, pia lishe duni kwa watoto inawaweka katika hatari ya kupata unene wa kupindukia baadaye, kisukari  na magonjwa mengine sugu ambayo yanaweza kusababisha matatizo ya kiafya maishani," amesema.

Afisa huyo amewashauri wazazi kuhudhuria kliniki na endapo mtoto atapata changamoto katika makuzi yake na ulaji kama kutoongezeka uzito, mtoto kukataa kula baadhi ya vyakula ni vyema mzazi apate ushauri kutoka kwa watoa huduma wa afya waliopo katika vituo vya afya nchini. 

UELEWA WA AKINA MAMA KUHUSU UNYONYESHAJI

Mkazi wa kijiji cha Mondo kilichopo kata ya Mondo Wilaya ya Chemba mkoani hapa Shakila Dossa  amesema kuwa  ananyonyesha  watoto wake hadi kufikia umri wa miaka miwili  kwa kuwa hana mimba na hana  tatizo lolote.

"Na nikijifungua mtoto wangu simpi chakula chochote hadi anapotimiza  umri wa miezi sita hata tunapoenda kliniki tunashauriwa na wataalamu wa masuala ya lishe," amesema.

Naye Hajara Mwenda  ni mama wa mtoto mmoja Mkazi wa Makole jijini hapa amesema mtoto wake alikataa kunyonya akiwa na umri wa mwaka miezi tisa   ambapo kwa sasa anampatia maziwa ya ng'ombe.

"Mwanangu alikataa kunyonya mwenyewe  na sababu inaweza kuwa ni kumuacha nyumbani kwa muda mrefu bila kunyonya kutokana na shughuli zangu za  kutembeza matunda, natoka asubuhi narudi jioni," amesema.

Ameongeza kuwa anafanya jitihada za kuhakikisha mwanae anapata lishe bora kwa kushauri wanaopatiwa  na Wataalamu wa masuala ya lishe wanapoenda kliniki.

WADAU WA LISHE

George Msalya ni Msajili wa Bodi ya Maziwa Tanzania (TDB),amewataka   wawazi wawapatie  watoto wao maziwa kwa kuwa yanavirutubisho vyote vinavyowakuza haraka ambavyo vikapatikana katika maziwa hayo.

Amesema mbali na vyakula vingine maziwa yanapatika haraka kwenye mwili mtoto akinywa baada ya saa mbili yanapatikana mwilini ambapo anapata  virutubisho na kwamba maziwa upatikanaji wapi pia ni rahisi.

Msajili huyo wa Bodi ya maziwa ameongeza kuwa watoto wanapokwenda shuleni na njaa uwezo wao wa kufikiri unakuwa mdogo muda mwingi atakuwa anarikiria njaa imayomsumbua.

" Tulichogua wakati tunatoa maziwa shuleni ni watoto kwenda shule bila kula, tunapotoa maziwa baada muda unaona mtoto amechangamka haraka," amesema Msalya.

Ameeleza kuwa wanagudua watoto wasio na virutubisho vya kutosha hata uwezo wa darasani unakuwa ni mdogo na kwa wale wanaokula vizuri hata darasani wanafanya vizuri.

Post a Comment

0 Comments

CHATANDA:RAIS DK. SAMIA AMEIMARISHA SEKTA YA MADINI