NAPE :TANZANIA IMEJIPANGA KUWA KITOVU CHA BIASHARA MTANDAO KATIKA UKANDA WA AFRIKA MASHARIKI NA KATI


Na  Asha Mwakyonde, Dodoma

RAIS Samia Suluhu Hassan amekuwa akifanya jitihada zinazochukuliwa na sekta ya Habari na Mawasiliano katika kuleta mabadiliko chanya ya kiuchumi hapa nchini.

Pia Amesema Wizara  ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari itahakikisha kuwa huduma za Posta nchini zinazidi kuboreshwa na kukua ili kuendana na mapinduzi ya teknolojia Duniani.

Hayo yamesemwa leo Januari 18,2023  jijini Dodoma na Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye wakati wa Maadhimisho ya 43  ya siku Posta Afrika yenye Kauli mbiu isemayo 'Posta Mwezeshaji Mahiri wa Biashara Mtandao inavyovuka Mikapa Barani Afrika' amesema Rais Samia ameonesha azma ya ziada katika kuendeleza matumizi ya mfumo wa Taifa wa anwani za makazi na postikodi. 

Waziri huyo ameeleza kuwa kwa kuanzia, Rais  Samia alihakikisha kuwa mfumo huo unatumika ipasavyo wakati wa utekelezaji wa Sensa ya Watu na Makazi iliyofanyika mwaka 2022.

Ameongeza kuwa Rais Samia amekuwa mstari wa mbele  kuunga mkono ujenzi wa jengo la makao makuu ya PAPU jijini Arusha; ambalo litakapokamilika, na kuanza kutumika, litaongeza ufanisi wa Umoja huo katika kutoa huduma ambalo litazalisha ajira zaidi kwa Watanzania.

Waziri Nape amesema Tanzania imejipanga kuwa kitovu cha biashara mtandao katika Ukanda wa Afrika Mashariki na Kati; na hatimae kufungua vituo vya pamoja vya huduma mbalimbali za Posta.

"Tanzania imejipanga kuwa kitovu ca biashara ya mtandao ambayo imekuwa kipaumbele cha Afrika yote, kama ilivyosisitizwa kwenye azimio la Afrika la mwaka 2020 kuhusu Kuibadili Afrika Kidijitali.  Azimio hili linataka kuwepo Soko Moja ya Kidijitali Afrika ifikapo mwaka 2030, ambapo hapatakuwa na mipaka ya watu, bidhaa, huduma na mitaji Barani humu, “ ameeleza.


Amefafanua kuwa kwa dhamira hiyo, Tanzania imetunga na kuweka mifumo ya kisera, kisheria na kiusimamizi inayolenga kuendeleza biashara mtandao nchini na kati yake na nchi nyingine Afrika.

Amesema kuwa hiyo ni pamoja na kuendeleza uwekaji na uendeshaji wa miundombinu katika maeneo yote yanayohusiana na biashara mtandao ma hilo hufanyika kupitia utoaji wa leseni na uwekaji wa sera zinazochangia biashara mtandao; kama vile Sera ya Teknolojia Hanari na Mawasiliano (Tehama) ya 2016 na kwamba kutunga Sheria ya Miamala Mtandaoni ya mwaka 2015 ambayo imeboreshwa mwaka 2022 lengo likiwa ni kuimarisha usalama na imani; vitu ambavyo ni muhimu kwenye shughuli za biashara mtandao.

Waziri huyo ameeleza kuwa wakati wanapoadhimisha miaka 43 ya Umoja wa Posta Afrika (PAPU) , Tanzania ina imani kuwa huduma za Posta zitawezesha kuibadili Afrika Kidijitali kama ilivyokusudiwa katika Azimio la Umoja wa Afrika (2020-2030). 

Pia ameongeza kuwa Tanzania imejipanga kuwa kitovu cha biashara mtandao katika Ukanda wa Afrika Mashariki na Kati; na hatimae kufungua vituo vya pamoja vya huduma mbalimbali za Posta.

Naye, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) Dk.Jabir Bakari amesema TCRA iko tayari kushiriki kikamilifu katika utatuzi wa changamoto zitakazojitokeza katika kuwezesha huduma mtandao hasa katika mipakani mwa nchi ya Tanzania. 

Kwa upande wake Meneja wa Posta Mkoa wa Dodoma Ferdinand Kabyemela kwa niaba ya Postamasta Mkuu amesema  Posta itaendelea kuwa mwezeshaji mahiri wa biashara zote za kuvuka mipaka na za mtandaoni (e-commerce) na zisizo za mtandaoni.

Post a Comment

0 Comments

CHATANDA:RAIS DK. SAMIA AMEIMARISHA SEKTA YA MADINI