ZAIDI YA KESI JINAI 17,411 ZA SAJILIWA MFUMO WA KIELEKTRONIKI


Na Asha Mwakyonde Dodoma

TAASISI za Umma zimetakiwa kuongeza matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA),lengo likiwa ni ufanisi na kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Hayo yamesemwa leo Agosti 23,2023  jijini Dodoma Waziri wa Nchi,Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora George Simbachawene, wakati wa hafla  ya makabidhoano ya mfumo wa kielektroniki wa kukusanya,kuchakata na kutunza kumbukumbu za kesi za jinai na tovuti ya Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS),uliotengenezwa na Mamlaka ya Serikali Mtandao (e-GA), 
kwa kushirikiana na ofisi hiyo.

Ameeleza kuwa hadi sasa zaidi ya kesi za jinai 17,411 zimesajiliwa katika  mfumo huo  kati ya kesi hizo kesi 7,361 zimeshafika mwisho na kutolewa hukumu na kwamba kesi 1050 zipo katika hatua mbalimbali za maamuzi.

Waziri Simbachawene amesema wanzishwaji wa mfumo huo ni utekelezaji wa maelekezo ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan aliyoyatoa Januari 31,mwaka huu wakati akizindua Tume ya kuangalia jinsi ya kuboresha Taasisi za Haki Jinai nchini,ambapo alielekeza umuhimu wa uwepo wa mfumo Jumuishi wa Haki Jinai na Mifumo kusomana.

"Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2025 na Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano (2021/22 -2025/26), yote inatambua nafasi ya TEHAMA katika kufikia malengo ya Taifa na hivyo kusisitiza  matumizi sahihi ya TEHAMA katika utekelezaji wa shughuli za Serikali na utoaji wa huduma kwa umma,"ameeleza.


Kwa upande wake Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Pauline Gekul amesema wao kama serikali dhamira yao ni kuona haki zote zinatolewa kwa wakati,huki akiamini  mfumo huo utakuwa chachu ya kufanikisha hilo na kurahisisha utendaji kazi.


Naye Mkurugenzi wa Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA),Benedict Ndomba amesema lengo la mfumo huo ni kurahisisha upatikanaji wa taarifa sahihi za uendeshaji wa mashtaka.



Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP), Sylivester Mwakitalu ameeleza kuwa mfumo huo ni nyenzo ya kurahisisha utendaji kazi wao na kwamba watautumia  kikamilifu ili kutoa matokeo chanya kwa wananchi na kwa wakati tofauti na awali.

Post a Comment

0 Comments

CHATANDA:RAIS DK. SAMIA AMEIMARISHA SEKTA YA MADINI