DK. MPANGO: SERIKALI IMEENDELEA KUKABILIANA NA UHARIBIFU WA MAZINGIRA, YAISISITIZA ELIMU YA KABONI


Na Asha Mwakyonde, Dodoma 

MAKAMU wa Rais Dk. Philip Mpango ameeleza kuwa Serikali imeendelea kukabiliana na uharibifu wa mazingira ikiwa ni pamoja na kuandaa Sera, kanuni, na upandaji miti na kwamba kampeni za usafi hasa mjini na kwenye fukwe lengo likiwa ni kuhamasisha utunzaji wa mazingira kupitia vyombo vya habari.

Pia Makamu wa Rais Dk. Mpango amesisitiza umuhimu wa utoaji elimu ya Biashara ya kaboni ambayo ni fursa katika kukabiliana na uharibifu wa mazingira na mabadiliko ya tabianchi. 

Dk. Mpango ameyasema hayo leo Septemba 9,2024 wakati akifungua Mkutano Maalum wa Viongozi, Wataalamu na Wadau wa Mazingira kuhusu Mwelekeo wa Mazingira Nchini amesema kuwa licha ya jitihada zinazofanywa na serikali kuondokana na uharibifu wa mazingira  bado Tanzania inalia hali ya mazingira sio nzuri.

Dk. Mpango ameongeza kuwa elimu inapaswa kutolewa kuhusu mikataba bora ya hewa ya kaboni iweje kwa maana ya mapato na teknolojia kutoka nchi zilizoendelea ambao ndiyo wazalishaji wakubwa wa hewa ya kaboni pamoja na kufahamu wajibu wa Jumuiya ya Kimataifa kwa nchi kama Tanzania ambazo zina Masinki makubwa ya Kaboni ikiwa ni pamoja na eneo kubwa la bahari na maziwa, ardhi oevu na eneo kubwa la hifadhi lililotengwa.

"Katika dhana ya uchumi wa buluu bado utafiti wa kutosha unahitajika unaolenga kubaini rasilimali nyingi zinazopatikana katika maji na menejimenti yake ikiwemo gesi asili, madini, viumbe hai pamoja na matumbawe," amesema.

Naye, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, Dk. Ashatu Kijaji, amesema kupitia mkutano huo mada mbalimbali zitajadiliwa ikiwamo ya biashara ya kaboni na inatarajiwa kuongeza hamasa ya uwajibikaji katika kukabiliana na uharibifu wa mazingira nchini.

Awali, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais, Zanzibar, Harusi Said Suleiman, amesema Zanzibar imeathiriwa na mabadiliko ya tabianchi kwenye mazingira na Agosti 17, mwaka huu walizindua program ya kuirudisha Zanzibar ya kijani.

Post a Comment

0 Comments

CHATANDA:RAIS DK. SAMIA AMEIMARISHA SEKTA YA MADINI