WAZIRI DKT. GWAJIMA AZINDUA MATAWI YA MASHABIKI WA SIMBA NA YANGA TARIME KUHAMASISHA KUPAMBANA NA VITENDO VYA UKATILI

Na WMJJWM-TARIME MARA

WAZIRI wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima amezindua matawi ya mashabiki wa timu za Mpira wa miguu za Simba na Yanga ikiwa na lengo la kuhamasisha jamii kupambana na vitendo vya ukatili na kujiletea maendeleo.

Akizungumza mara baada ya kuzindua matawi hayo Septemba 16, 2024 katika Kata ya Ganyange Wilayani Tarime mkoani Mara amepongeza ubunifu huo kwa kujumisha masuala ya michezo katika kupambana na vitendo vya ukatili.

Ameupongeza uongozi wa Wilaya ya Tarime kwa kushirikiana na Shirika Lisilo la Kiserikali la Kivulini kwa kujumuisha Jamii hiyo katika kupeana elimu ya kupambana na vitendo vya ukatili na kutumia fursa mbalimbali za kiuchumi.

"Niwapongeze kwa ubunifu huu wa kutafsiri ushabiki wa mchezo wa Mpira wa miguu katika kuunga mkono juhudi za Serikali na wadau katika kupambana na vitendo vya ukatili, Hongereni sana katika hili" amesema Waziri Dkt. Gwajima.

Aidha amewapongeza mashabiki wa timu hizo kuunga mkono jitihada za Rais Samia Suluhu Hassan za kuendeleza na kuhamasisha michezo kwa kuunga hamasa goli la Mama katika mashindano ya Kimataifa kwa wao kuunga nguvu zao katika kupambana na vitendo vya ukatili na kutumia fursa mbalimbali za kiuchumi.

Pia amewahakikishia viongozi wa matawi hayo ushirikiano kutoka kwa Wizara na kuwaomba kupeleka ubunifu huo katika Kata nyingine na Wilaya za Mkoa wa Mara ili kuwa na nguvu moja ya kupambana na vitendo vya ukatili.

"Nitoe rai kwa Viongozi, Maafisa Maendeleo ya Jamii, Maafisa Ustawi wa Jamii na wadau wengine kuendelea kubadilisha fikra za Jamii ili iachane na dhana na Mila zlzisizo za wakati huu ili kusaidia Jamii kujikita katika maendeleo" amesisitiza Waziri Dkt. Gwajima.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Tarime Meja  Edward Gohele amemuahidi Waziri Dkt Gwajima kuendelea kutumia njia ya mashabiki wa timu za Simba na Yanga kufikisha ujumbe wa kupambana na vitendo vya ukatili katika Wilaya mzima ya Tarime na Mkoa wa Mara kwa ujumla.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Shirika la Kivulini Yassin Ali amesema Shirika hilo liliona umuhimu wa Jamii yenyewe katika kupeana elimu ya kupambana na vitendo vya ukatili hivyo wakaja na njia ya kutumia mashabiki wa Simba na Yanga ili kufikisha kwa haraka elimu ya kupambana na vitendo vya ukatili na fursa za kiuchumi.

Nao baadhi ya mashabiki wa Simba na Yanga wamemshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea Kuimarisha sekta ya michezo nchini kwa kuhamasisha kupitia goli la mama hivyo wao wameunga mkono juhudi hizo kwa kutumia sekta hiyo kutatua changamoto za kijamii zikiwemo ukatili wa kijinsia.

Post a Comment

0 Comments

CHATANDA:RAIS DK. SAMIA AMEIMARISHA SEKTA YA MADINI