MASHAMBA DARASA 100 YA MALISHIO YAMEANDALIWA KUWAONESHA WAFUGAJI


Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Sekta ya Mifugo) Tixon Nzunda.

Baadhi ya wadau wakimsikiliza Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi( Sekta ya Mifugo).

Na Asha Mwakyonde, Dodoma 

KATIBU  Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi,(Sekta ya Mifugo), Tixon Nzunda amesema serikali kupitia Wizara hiyo  imeandaa mashamaba darasa 100 ya malishio ya mifugo kwa ajili ya kuwaonyesha wafugaji namna ya kuzalisha malighafi hiyo kwa ajili ya mifugo lengo  likiwa ni kuongeza tija katika uzalishaji.

Hayo ameyasema jijini hapa Leo Novemba 29,2022 wakati akifungua kikao cha wadau cha maboresho ya kodi na tozo katika sekta ya mifugo amesema mashamba hayo ni  maalumu kwa ajili ya kuwaonesha wafugaji wadogo namna ya kufuga na pamoja na kuwa na malisho ili kuokoa mifugo katika kipindi cha hali mbaya ya ukame , njaa na dharura.

Katibu huyo amefafanua kuwa  lengo jingine la kuandaa mashamba hayo ni kuongeza tija ya uzalisaji wa malisho kwa wafugaji na kuondoa dhana ya utegemezi.

”Tumeamua kuwekeza  kila mmoja atambue hili  lengo ni wafugaji wetu wapate faidaa na kuona serikali ina wajibu wa kufanya kila kitu kwa ajili yao.

Nzunda ameongeza kuwa  kikao hicho ni ha kujengea  uelewa wa pamoja kwa kupitia maombi ya kufuta tozo na kodi mbalimbali zilizoombwa mwaka huu wa fedha  na  kujadili maombi mapya.

Amesema wafugaji  ni lazima watambue kodi na tozo ni vyanzo vikuu vya mapato hivyo  umakini usipotumika serikali itapoteza mapato yake na Taifa likakosa fedha ya kutoa huduma muhimu kwa wananchi wake.

“Tumekuwa na desturi ya kuomba kodi na tozo mbalimbali zipunguzwe au kufutwa lakini ni vyema tukawa na utamaduni pia wa kuleta mapendekezo ya namna serikali itakavyoweza kupata vyanzo vipya vya mapato kutoka kwenye sekta yetu ya mifugo,”amesema.

Amesema mwaka jana kuliwasilishwa maombi ya kupunguza au kufutiwa kodi na tozo 45 kati ya hizo maombi 42 yalikubaliwa  kwa kupunguzwa au kufutwa kabisa.

Aidha Katibu huyo ameishukuru  serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan kwa kupunguza kodi na tozo tulizoziomba mwaka jana na kupelekea kuongeza biashara ya ndani na nje ya nchi kwenye sekta ya mifugo.

Kwa upande wake Mdau wa sekta ya mifugo ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti Baraza la Kilimo Tanzania (ACT), Jitu Viajlal Son amesema katika kikao hicho watajadili changamoto mbalimbali ambazo wanakumbana nazo na kuziwasilisha kwa katibu Mkuu kwa ajili ya kupatiwa ufumbuzi.

Amesema kumekuwa na changamoto ambazo zimekuwa zikiwakabili na nyingine ikiwemo suala la kodi na tozo ambazo zinahitaji maamuzi ya juu.

“Kikao hiki ni muhimu kwetu naamini tutatoka na maadhimio ya pamoja ambayo yataboresha sekta hii na kuleta matokeo chanya kwa wafugaji na taifa kwa ujumla, pamoja na kuongeza tija katika uzalishaji wa bidhaa zitokanazo na mifugo,”amefafanua.


Post a Comment

0 Comments

ENDELEENI KUCHUKUA TAHADHARI DHIDI YA VIRUSI VYA UKIMWI” MHE. NDERIANANGA