SERIKALI YAJIVUNIA CHUO CHA UONGOZI WA MAHAKAMA LUSHOTO



Mhe. Dkt. Damas Daniel Ndumbaro, Waziri wa Katiba na Sheria akihutubia Watumishi wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto alipofanya ziara ya Chuoni hapo.

Baadhi ya Watumishi wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama wakifuatilia hotuba ya Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro alipofanya ziara chuoni.


Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo na Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mheshimiwa Dkt. Gerald A. M. Ndika akitoa salamu za awali kabla ya kumkaribisha Mgeni Rasmi.


Mhe. Dkt. Damas Daniel Ndumbaro, Waziri wa Katiba na Sheria akipanda mti kwenye bustani ya Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto.
Picha ya pamoja ya meza kuu na wajumbe wa Menejimenti ya Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto pamoja na waumishi wa chou hicho.

Lusajo Mwakabuku  na Felix Chakila - WKS

WAZIRI wa Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro amesema Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto - IJA ni chuo cha mfano wa kuigwa katika utoaji wa mafunzo elekezi ya awali na mafunzo endelevu ya kimahakama kwa kuzingatia Sera ya Mafunzo ya Mahakama ya Mwaka 2019 ambayo inakitambua Chuo hicho kama kitovu au kisima cha utoaji mafunzo kwa watumishi wa Mahakama.

Dkt. Ndumbaro ameyasema hayo Tarehe 6 Machi, 2023 alipotembelea Chuo hicho na kuzungumza na Uongozi wa Chuo, Menejimenti ya watumishi na Wafanyakazi wa IJA na kuongeza kwamba Wizara ya Katiba na Sheria inajivunia kwa uwepo wa chuo hicho ambacho kimebeba taswira ya nchi hususan kwa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki ambapo kimeendelea kuwa mfano wa kuigwa kama Chuo kinachojenga na kuimarisha kada ya Sheria.

“Chuo hiki kweli ni kitovu na kisima cha elimu bora. Kimsingi, chuo kina uwezo wa kujenga  taaluma  na kuwanoa wataalam mbalimbali wa Sheria wanaokwenda kusimamia haki wakiwemo Mahakimu na watumishi wengine wa mahakama.” Alisema Dkt. Ndumbaro.

Akizungumza mara baada ya kukagua mazingira ya chuoni hapo yakiwemo mabweni, Mhe. Dkt. Ndumbaro amebainisha kuwa Chuo hicho kimekuwa kikifanya kazi nzuri kwa kutoa mafunzo mbalimbali elekezi na endelevu kwa watumishi wa Mahakama ya Tanzania yakiwemo mafunzo elekezi kwa Mahakimu wote mara wanapoajiriwa kujiunga kwa mara ya kwanza na utumishi wa Mahakama kwa lengo la kuwajengea uwezo wa kutenda haki kwa wote na kwa wakati kwa kuzingatia misingi ya sheria na uadilifu.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo na Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mheshimiwa Dkt. Gerald A. M. Ndika amesema Chuo kimekabidhiwa majukumu ambayo ni kutoa mafunzo, kufanya tafiti na kutoa huduma za kitaalamu majukumu ambayo Chuo kimemudu kuyatekeleza kwa ufanisi.

Tangu kuanzishwa kwa Chuo hicho, mhimili wa Mahakama ndiyo mnufaika mkubwa wa zao la kitaaluma la Chuo hcho kwani mhimili huu umeweza kuendeleza watumishi wake pamoja na kuajiri Mahakimu na watumishi wengine kutoka katika Chuo hiki. Chuo cha IJA pia kimekuwa kikiratibu na kufanya mafunzo endelevu ya kujengea uwezo watumishi mbalimbali wa Mahakama.

Katika ziara hiyo, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro aliambatana na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Dkt.Khatibu Kazungu na kupokelewa Uongozi wa Chuo ukiongozwa na Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo na Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mheshimiwa Dkt. Gerald A. M. Ndika na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Paul F.Kihwelo.

Post a Comment

0 Comments

CHATANDA:RAIS DK. SAMIA AMEIMARISHA SEKTA YA MADINI