ARCH KONDORO: TBA KUNA MIRADI MINGI AMBAYO IPO KATIKA HATUA YA UTEKELEZAJI


Na Asha Mwakyonde,Dar es salaam

WAKALA wa Majengo Tanzania (TBA),imesema ina miradi mingi ambayo ipo katika hatua za utekelezaji  ambayo inatarajiwa kuanza utelezaji wake mara baada ya fedha za  bajeti ya mwaka huu zitakapoingia.

Akizingumza jijini Dar es salaam Julai 11,2023 Mtendaji Mkuu wa TBA, Arch. Daud Kondoro,katika Maonesho ya 47 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (DITF),maarufu Saba Saba, yenye kaulimbiu isemayo"Tanzania Mahali sahihi pa Biashara na Uwekezaji,"amesema wakala wa majengo ni moja ya Taasisi ambazo zipo nchini ya Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi na kwamba bajeti ya fedha ya mwaka huu tayari imeshapitishwa hivyo kuna miradi kadhaa ambayo imeshapitishwa na wanatarajia kuanza kutekeleza mara fedha zitakapoingia.

Amesema miradi hiyo ipo  katika mikoa ya Mwanza, Arusha pamoja na Dar es salaam na kwamba katika maonesho ya mwaka ujayo watakuwa na miradi mingi ambayo wanatarajia kuionesha.

Mtendaji huyo ameongeza kuwa wana miradi ambayo wanaitekeleza kupitia fedha za ndani, kupitia kurugenzi walizonazo ikiwamo ya ushauri ambapo kuna fedha ambazo wanazipata  wanapotekeleza miradi hiyo kama sehemu ya malipo, ya ujenzi na makusanyo ambayo wanayoyapata kutokana na kodi ya pango.

"Fedha hizi tunazikusanya na kuzitumia katika utekelezaji wa mradi mbalimbali ambayo ni ya kuhakikisha kunakuwa na majengo bora kwa ajili ya watumishi wa Umma hapa nchini," ameongeza.

Bajeti zote zilizopita kuna sehemu inahusu majengo na tunatengemea kupitia mfumo mpya ambao umeanzishwa kupitia manunuzi tutaendelea kufuatilia na kuhakikisha tunapata zabuni mbalimbali ambazo zitakuwa ya ushauri na ujenzi, matarajio yetu ni kuwa na mambo makubwa kipindi kinachokuja cha maonesho haya," amesema.

Ameeleza kuwa wanatarajia kuwa na ujenzi mkubwa mkoani Arusha eneo la Kaloleni wa nyumba za watumishi wa Umma na kwamba katika ujenzi huo  watatumia fedha za ruzuku kwa bajeti ya mwaka uliopita pamoja na makusanyo ya ndani.

Arch.Kondoro, ameongeza kuwa wana mradi wanaoendelea nao wa Temeke kota ambapo wanatarajia kujenga bloku saba za nyumba na kila bloku hizo zitakuwa na familia 144 na tayari wameanza moja.

" Nashukuru nimepata nafasi ya kufika kuzunguka na nimeangalia banda letu ni zuri linataarifa za kutosha kuhusu miradi mbalimbali ambayo wakala wanatekeleza na nimefurahi kupata maelezo kutoka kwa watumishi wa wakala wa majengo naendelea kuwatia moyo kwa kazi kubwa ambayo wanaoifanya," amesema.

Lengo la kuanzishwa kwa TBA ni kwa ajili ya kujenga nyumba za viongozi na watumishi wa Umma.

Post a Comment

0 Comments

 KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA UTAWALA, KATIBA NA SHERIA YANOLEWA