WAHADHIRI DIT WAJENGEWA UWEZO KUHUSU MILIKI UBUNIFU

Dar es salaam

WAKALA wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), leo Mei 26,2023 imetoa elimu kwa Wahadhiri wa Chuo Cha Teknolojia Dar es Salaam (DIT), kwa lengo la kuwajengea  uwezo kuhusu Milki Ubunifu (IP).

Elimu hiyo imetolewa katika Ofisi za BRELA ambapo Wahadhiri hao walifika na kupata fursa ya kujifunza uchakataji wa maombi ya Alama za Biashara na huduma pamoja na Hataza.

Akizungumza kwa niaba ya Afisa Mtendaji Mkuu, Kaimu Mkurugenzi wa Miliki Ubunifu Bi. Loy Mhando amebainisha kuwa amefurahishwa na ugeni huo kwa kuwa unaonesha dhamira yao ya dhati ya kuhitaji kufahamu zaidi kuhusu huduma zinazotolewa na BRELA.

“Mara nyingi Taasisi imekuwa ikifanya jitihada kuwafuata wadau wake katika maeneo yao ili kuwapatia elimu, kitendo cha kufika katika Ofisi za BRELA kimeonesha dhamira ya dhati na kiu ya kujifunza kuhusu huduma zinazotolewa hapa. Ni imani yangu kwamba elimu mtakayoipata hapa itawasaidia katika majukumu yenu ya kila siku”, amefafanua Bi. Mhando.

Naye Mkuu wa Sehemu ya Alama za Biashara na Huduma kutoka BRELA, Bw. Seka Kasera ameeleza kuwa mbali na Usajili wa Alama za Biashara na Huduma pamoja na  utoaji wa Hataza, Taasisi pia inatoa huduma nyingine nne.

Amezitaja huduma hizo kuwa ni Usajili wa Kampuni, Majina ya Biashara, utoaji wa Leseni za Biashara kundi “A” na Leseni za Viwanda na kusisitiza kuwa huduma zote kwa sasa zinatolewa kwa njia ya mtandao.

Wahadhiri hao wamefanya ziara hiyo ya mafunzo ili kuongeza maarifa yatakayo wawezesha kuwafundisha wabunifu waliopo katika chuo hicho, ili wanapozalisha bunifu mbalimbali wazilinde kisheria na kunufaika na bunifu hizo.

Post a Comment

0 Comments

 MAGARI 25 YA TUME YA MADINI YAMEZINDULIWA,YATASAMBAZWA KWENYE OFISI ZA MAAFISA MADINI