RAIS. DK. SAMIA AITAKA WIZARA YA KILIMO KUANGALIA VYAMA VYA USHIRIKA, KUKUTANA NA MAAFISA USHIRIKA

Na Asha Mwakyonde, DODOMA 

RAIS Dk. Samia suluhu Hassan ameitaka Wizara ya Kilimo kutupia jicho Sekta ya Vyama vya Ushirika ili kurejesha hadhi na mchango wa ushirika nchini lengo likiwa ni kuleta mageuzi makubwa katika Sekta hiyo.

Pia Rais Dk.Samia amesema kuwa anatafuta siku akutane na maofisa ushirika ili akae nao wawekuelewana kwa karibu zaidi.

Haya ameyasema leo Agosti 8,2024 wakati wa kilele cha sikukuu ya wakulima na Wafugaji ambayo imefanyika Kitaifa kwenye viwanja vya Nzuguni jijini Dodoma yenye kauli mbiu isemayo "Chagua Viongozi Bora wa Serikali za Mitaa kwa Maendeleo Endelevu ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi".

Rais Samia ameeleza mageuzi yaliyofanywa katika sekta hizo, miradi inayoendelea pamoja na kutoa maelekezo kwa watendaji na kuitafsiri kaulimbiu ya maadhimisho ya mwaka huu.

Amesema kuwa mageuzi makubwa ambayo yanafanywa na serikali kwenye sekta za kilimo, mifugo na uvuvi ili yalete matokeo ya uchumi endelevu ni lazima kujenge vyama vya ushirika vilivyo imara.

"Natafuta siku nikutane na maofisa ushirika nikae nao tuelewane kwa karibu zaidi, " ameeleza Rais Dk. Samia.

Ameongeza kuwa serikali imepiga hatua kubwa ambazo zimeanza kuleta matokeo mazuri na kwamba dhamira yake ni kujenga uchumi jumuishi katika sekta hizo muhimu.

Akizungumzia ukuaji wa sekta ya kilimo Rais Samia ameeleza kuwa mwaka 2023 sekta hiyo imekua kwa asilimia 4.2 ambapo imechangia asilimia 26.5 katika Pato la Taifa na kutoa ajira kwa wananchi kwa asilimia 65.6 huku akichangia upatikanaji wa malighafi za viwandani kwa asilimia 65.


Rais Dk Samiaa akizungumzia ukuaji huo wa sekta ya kilimo amesema imechangia kuongeza mauzo ya nje kwa asilimia 30 na kuhakikisha nchi inakuwa na utoshelevu wa chakula kwa zaidi ya asilimia 100.

Ameongeza kuwa kiwango cha uzalishaji wa mazao ya chakula kimeongezeka kutoka tani milioni 17.1 (2021/2022) hadi kufikia tani milioni 20.4 (2023/2024) sawa na asilimia 19.

Rais Dk. Samia amehitimisha Sikukuu ya Wakulima, Wafugaji na Wavuvi (Nanenane) kwa mwaka 2024.

Post a Comment

0 Comments

CHATANDA:RAIS DK. SAMIA AMEIMARISHA SEKTA YA MADINI